Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uwekezaji mkubwa unahitajika kutatua tatizo la chakula Asia:Diouf

Uwekezaji mkubwa unahitajika kutatua tatizo la chakula Asia:Diouf

Mtaalamu wa chakula wa Umoja wa Mataifa leo ameonya kuwa watu takriban milioni 650 barani Asia wanakabiliwa na njaa na hali hiyo itaendelea.

Mtaalamu huyo ambaye ni mkuu wa shirika la chakula na kilimo FAO Jacques Diouf amesisitiza kwamba ingawa bei ya chakula imeshuka tangu wakati wa tatizo la kimataifa la chakula 2008, tatizo la utapia mlo linazidi kuwa baya na serikali za Asia haziwekezi vya kutosha katika kilimo.

Akizungumza katika mkutano wa kimataifa wa usalama wa chakula mjini Manila, amesema kwamba zaidi ya Waasia milioni 60 walipata utapia mlo mwaka jana na kuongeza idadi ya walio na utapia mlo katika ukanda huo kufikia milioni 642. Amesema tatizo la kukosa chakula ni matokeo ya kutotoa kipaumbele katika sera za kilimo kwenye nchi zinazoendelea.