Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Katika Siku ya Wakimbizi Duniani UM umeonya kwamba wengi hawawezi kurejea nyumbani

Katika Siku ya Wakimbizi Duniani UM umeonya kwamba wengi hawawezi kurejea nyumbani

Juni 20 ni Siku ya Wakimbizi Duniani na kauli mbiu ya mwaka huu ni "nyumbani" ikimaanisha haja ya wakimbizi hao kuwa na mahali wanapopaita nyumbani.

Kamishina Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudunia wakimbizi UNHCR Antonio Guterres anasema licha ya kupungua idadi ya wakimbizi wanaorejea nyumbani kwa hiyari shirika hilo linafanya kila juhudi kupata suluhisho.

Mwaka jana zaidi ya wakimbizi 128,000 walipelekwa kwa ajili ya kuanza maisha mapya kutoka nchi zao walizoomba ukimbizi kwa mara ya kwanza. Na wengi hupelekwa kwenye nchi zilizoendelea ambako inakuwa rahisi kuanza maisha mapya. Na idadi hiyo ni mara mbili ya idadi ya mwaka 2005. Kutokana na wema wa nchi kama Tanzania wakimbizi zaidi ya 162,000 wa Burundi walioingia Tanzania 1972 walipatiwa uraia na sasa ni Watanzania.

Ujumbe maalumu wa wakimbizi kwa mwaka huu ni kwamba watu wanaweza kuwapokonya nyumba zao lakini hawawezi kuwapokonya maisha yao ya baadaye.