Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM umemuenzi aliyekuwa Rais wa Nigeria Umaru Yar'Adua

UM umemuenzi aliyekuwa Rais wa Nigeria Umaru Yar'Adua

Mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa leo umekutana kumkumbuka aliyekuwa Rais wa Nigeria Umar Yar\'Adua ambaye alifariki dunia wiki iliyopita.

Wawakilishi wa makundi mbalimbali kwenye mkutano huo wametoa taarifa zao kuhusu Rais huyo na rambirambi zao kwa familia yake, serikali ya Nigeria wa watu wa taifa hilo.  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema wakati wa uhai wake kwa muda mfupi aliokuwa madarakani Rais huyo alitimiza majukumu yake kwa ari na moyo wote huku akiheshimu haki za wote.

Ban ameongeza kuwa atakumbukwa kwa kwa mchango wake wa uongozi wa kidemokrasia, kufufua uchumi na hususani juhudi zake za kurejesha amani kwenye jimbo la utajiri wa mafuta nchini Nigeria la Niger Delta .Kama mwenyekiti wa jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika ya Magharibi ECOWAS Ban amesema Yar Adua alipambana bila kuchoka kupinga mabadiliko yasiyokuwa ya kikatiba kwenye serikali na kuhakikisha amani inapatikana kwenye ukanda mzima."

Ban pia amesema anamshukuru marehemu Rais huyo kwa kuzingatia misingi na malengo ya Umoja wa Mataifa, ikiwemo mchango wa vikosi vyake katika operesheni za Umoja wa Mataifa za kulinda amani. Leo Rais wa mpito Goodluck Jonathan amemteua gavana wa jimbo la Kaduna Namadi Sambo kuwa makamu mpya wa Rais wa nchi hiyo.