Rais Kabila kupambana na maambukizi ya HIV kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto DRC
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Joseph Kabila amewahakikishia maafisa wa ngazi za juu wa Umoja wa Mataifa niya yake ya kuchangia katika kuwepo kwa kizazi kisicho na ukimwi pamoja na kuhakikisha wanazuia maambukizi ya virusi vya HIV kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, katika nchi yake na katika mataifa mengine pia.
Rais Kabila akizungumza na mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu , UNFPA, Thoraya Ahmed Obaid na Mkurugenzi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupamabana na Ukimwi, UNAIDS, Michel Sidibe, amesema hayo ni maswala muhimu kwa watoto na akina mama wa taifa lake.
Rais Kabila ameongezea kusema kuwa ataongoza katika kuhakikisha kunakuwepo na kizazi kisichokuwa na ukimwi na kuahidi kuanzisha mpango wa kupunguza hali ya maambukizi nchini humo.Pia amesema atatumia nafasi yake ya kuwa mwenye kiti wa jumuiya ya mataifa ya Kusini mwa Afrika SADC kwa kuwashawishi viongozi wenzake kuunga mkono mpango huo.