Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban kutuma ujumbe Kyrgystan baada ya upinzani kutangaza kushika hatamu

Ban kutuma ujumbe Kyrgystan baada ya upinzani kutangaza kushika hatamu

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ametangaza kwamba anamtuma mjumbe maalumu kwenda Kyrgystan ambako ghasia zimeongezeka na upinzani umetangaza kushika hatamu za uongozi.

Mjumbe huyo ni Jan Kubis ambaye ni katibu mkuu wa tume ya Umoja wa Mataifa ya uchumi kwa nchi za Ulaya UNECE. Viongozi wa upinzani nchini humo wamewaomba wananchi kujitokeza kuwazuia viongozi wa serikali kutoroka nchini baada ya kutangaza mapinduzi.

Hatua ya kupindua serikali ilitokea jana kufuatia maandamano na ghasia kubwa ambazo zimesababisha vifo vya watu zaidi ya 40. Viongozi hao wanamshutumu Rais Kurmanbek Bakiyev kukandamiza upinzani . Wapinzani hao wamesema watashikilia madaraka kwa miezi sita ili kuweza kuunda katiba mpya. Kiongozi wa upinzani anayeshikilia serikali kwa sasa ni Bi Roza Otunbayeva na anamtaka Rais Bakiyev kujiuzulu.