Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Leo ni kumbukumbu ya miaka 16 tangu mauaji ya Kimbari ya Rwanda 1994

Leo ni kumbukumbu ya miaka 16 tangu mauaji ya Kimbari ya Rwanda 1994

Loe ni miaka 16 tangu kufanyika mauaji ya kimbari yaliyoitia simanzi dunia mwaka 1994 nchini Rwanda ambapo watu zaidi ya laki nane waliuawa na wengine kwa maelfu kuwa wakimbizi.

Siku hii inakumbukwa kote duniani na kwenye Umoja wa Mataifa hafla zinafanyika kwenye ofisi zake mbalimbali. Hapa New York hotuba inatolewa na naibu Katibu Mkuu wa umoja wa Mataifa Asha Rose Migiro, mwakilishi wa Rwanda kwenye Umoja wa Mataifa na manusura wa mauaji hayo.

Katika ujumbe maalumu wa kumbukumbu ya leo Katibu mkuu Ban Ki-moon amesema Umoja wa Mataifa umejizatiti kuhakikisha haki inatendeka kwa waathirika wa mauaji hayo na kuzuia asilani yasitokee tena.

Tangu kutokea kwa mauaji hayo watu kadhaa wameshafikishwa kwenye mahakama inayoshughulikia kesi za mauaji hayo ya ICTR Arusha Tanzania na kuhumiwa, na washukiwa wengine wangali wanatafutwa.