Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa wawakumbuka wafanyakazi wake waliokufa Haiti

Umoja wa Mataifa wawakumbuka wafanyakazi wake waliokufa Haiti

Wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa na familia za watu 101 waliofariki dunia katika tetemeko la Januari nchini Haiti, leo wamekusanyika katika makao makuu ya UM mjini New York kuwakumbuka wahanga hao na pia kukumbuka pigo kubwa kabisa la kupoteza watu wengi kwa mara moja katika historia ya Umoja wa Mataifa.

Katibu Mkuu wa UM Ban Ki-moon ni miongoni mwa waliohudhuria kumbukumbu hiyo, pamoja na maafisa wengine wa ngazi za juu wa UM, wawakilishi wa nchi wanachama wa UM na wafanyakazi wa mpango wa UM nchini Haiti MINUSTAH.

Tetemeko hilo la Januari 12 lilisambaratisha kabisa makao makuu ya UM nchini Haiti na majengo mengine yaliyokuwa na ofisi za Um mjini Port-au-Prince. Miongoni mwa waliofariki dunia ni pamoja na mwakilishi maalumu wa UM Haiti Hedi Annabi na naibu wake Luiz Carlos da Costa.