Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Katibu mkuu wa UM ahofia mauaji yaliyotokea Nigeria

Katibu mkuu wa UM ahofia mauaji yaliyotokea Nigeria

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban ki-moon amesema anahofia ghasia za kidini katika mji wa Jos nchini Nigeria ambazo zmekatili maisha ya mamia ya watu.

Kwa mujibu wa duru za habari nchini humo watu waliokuwa na mapanga kutoka milima ya jirani walivamia vijiji katika eneo hilo mwishoni mwa wiki na kuwachinja wanawake, watoto na wazee ambao hawakuweza kukimbia. Katibu mkuu Ban ki-moon amesema hii ni hali mbaya ambayo viongozi wa Nigeria wanatakiwa kuipatia ufumbuzi.

Amesema "Nina hofu juu ya ghasia zaidi za kidini ambazo zinasababisha kupoteza maisha ya watu. Nitaziomba pande zote husika kurejesha hali ya utulivu, Viongozi wa kisiasa na kidini nchini Nigeria lazima washirikiane kupata ufumbuzi wa chanzo na suluhisho la kudumu la machafuko ya Jos".

Jos ni mji ulioko katikati ya eneo la Kaskazini linalokaliwa na Waislamu wengi na la kusini lenye Wakristo wengi nchini Nigeria na limekuwa chachu ya machafuko ya kidini nchini humo.