Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

ICRC yasaidia kuachiliwa huru askari sita Congo DRC

ICRC yasaidia kuachiliwa huru askari sita Congo DRC

Katika operesheni mbili tofauti zilizofanyika jana na leo kamati ya kimataifa ya msalaba mwekundu (ICRC) imesaidia katika kuachiliwa na kusafirishwa kwa wanajeshi sita wa jeshi la Congo waliokuwa wanashikiliwa na makundi yenye silaha katika majimbo ya Kivu ya Kusini na Kaskazini.

Pande husika ziliomba ICRC kushughulikia kuachiliwa kwao kama mpatanishi. Mjumbe wa ICRC alizungumza na kila mmoja wa askari hao ili kuhakikisha kwamba wanakubali kwa hiyari kurejeshwa katika jeshi la Congo. Franz Rauchenstein mkuu wa ujumbe wa ICRC nchini Congo amesema, "Tumefurahishwa na operesheni hizi ambazo zinaonyesha imani yaliyonayo makundi yanayozozana congo kwa ICRC. Na imani hii ndio imetusaidia kutimiza wajibu wetu kama wapatanishi. Ingawa hali ya usalama katika majimbo ya mashariki mwa nchi hiyo ikiwemo Orientale, na Equateur bado inatia mashaka."

Mashariki mwa Congo hali bado ni ya wasiwasi na hasa maeneo ya vijijini na kwa hivyo ni muhimu kuhakikisha juhudi za kila aina zinafanyika kuhakikisha sheria za kimataifa za masuala ya kibinadamu zinafuatwa.