Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mwanaharakati wa Kenya juu ya Mazingira awakilisha maoni binafsi juu ya Mkutano wa Copenhagen

Mwanaharakati wa Kenya juu ya Mazingira awakilisha maoni binafsi juu ya Mkutano wa Copenhagen

Majadiliano ya Mkutano Mkuu wa Copenhagen, unaojulikana kama Mkutano wa COP15, yaliendelezwa kwa wiki mbili, kwa kasi ambayo wajumbe wengi, hasa wale wa kutoka nchi zinazoendelea, walilalamika ilikuwa ni ya polepole sana, hali ambayo iliwakatisha tamaa juu ya uwezekano wa kufikia mapatano ya mwisho yanayoridhisha.

Wajumbe hawa wa nchi zinazoendelea wanaamini suluhu ya itifaki ziada, ya kudhibiti bora athari za hali ya hewa, haina dalili njema kupatikana kwenye Mkutano wa COP15. Kama inavyoeleweka, mataifa yanayoendelea ni maeneo yenye kudhurika zaidi kimazingira, kwa sababu ya hali ya hewa ya kigeugeu, ambayo haifuati majira, na huchochea matatizo ya kila aina, ikijumlisha mvua kali na mafuriko, na ukame wa muda mrefu wa usioshuhudiwa kihistoria.

Kwenye mahojiano yaliofanyika kati ya wiki na waandishi habari, KM Ban Ki-moon alikiri majadiliano ya Copenhagen, kati ya wajumbe wa kimataifa, yalifanyika kwa kasi iliodorora na iliochelewesha suluhu ya mapema kupatikana. Alikumbusha KM ya kuwa mfumo wa mashauriano na majadiliano ya Mkutano wa Copenhagen yalikuwa "ni moja ya mazungumzo magumu sana kusimamiwa na UM" kihistoria. Lakini, hata hivyo KM aliamini  mapatano ya kuridhisha yatapatikana mwisho wa majadiliano ya Mkutano wa Copenhagen.

Miongoni mwa wajumbe wa kimataifa waliohudhuria Mkutano wa Copenhagen alikuwemo kijana wa kutoka Kenya, aliyewakilisha Mradi wa Vijana wa Afrika juu ya Mabadiliko ya Hali ya hewa, anayeitwa Sylvia Wachira. Mwandsishi habari wa Idhaa ya Kichina ya Redio ya UM, LiLing Huang, ambaye anawakilisha Idara ya Habari ya UM (DPI) mkutanoni Copenhagen, alipata fursa ya kumhoji Sylvia Wachira.

Endelea na taarifa yetu kwa kusikiliza mahojiano kamili kwenye idhaa ya mtandao.