Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Shughuli za Baraza la Usalama kwa Alkhamisi

Shughuli za Baraza la Usalama kwa Alkhamisi

Mapema asubuhi ya leo, Baraza la Usalama limepitisha azimio la kuongeza muda wa shughuli za Ofisi ya UM juu ya Mchanganisho wa Huduma za Amani Burundi (BINUB) ambazo zinatazamiwa kuendelezwa hadi mwisho wa mwaka 2010.

Vile vile Baraza la Usalama limepitisha azimio la kuongeza, kwa miezi kumi na mbili zaidi, vikwazo vya kusafiri nje, dhidi ya baadhi ya raia wa Liberia, na ilipendekezwa Tume ya Wataalamu wanaohusika na vikwazo katika Liberia nayo pia muda wake wa kazi uendelee mpaka tarehe 20 Disemba 2010. Halkadhalika, Baraza limepitisha azimio la kurekibisha miongozo kuhusu orodha ya watu, vitengo na taasisi zinazodaiwa kufungamana na harakati za makundi ya al-Qaeda na Taliban. Mongoni mwa marekibisho yaliopendekezwa ni ile rai ya kuanzisha Ofisi ya Uchunguzi wa Malalamiko, itakayoendeleza huduma zake, awali, kwa miezi 18, na itasailia majina yanayostahiki kufutwa kutoka orodha ya watu na taasisi zinazodaiwa kuhusika na makundi ya al-Qaeda na Taliban.