Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mjumbe wa UM apongeza usajili wa amani wa wapiga kura Sudan

Mjumbe wa UM apongeza usajili wa amani wa wapiga kura Sudan

Mjumbe Mkuu wa UM kwa Sudan, Ashraf Jehangir Qazi, ametangaza kukaribisha mwisho mzuri, wa utaratibu wa kusajili wapiga kura, kwa uchaguzi wa vyama vyingi, utakaofanyika nchini Sudan mwaka ujao. Asilimia 75 ya watu waliofikia umri wa kupiga kura walirajisiwa, sawa na raia wa Sudan milioni kumi na tano. Baina ya tarehe 1 Novemba mpaka Disemba 07 (2009), mamilioni ya watu walifanikiwa

kujiandikisha kupiga kura katika vituo vilivyoenezwa, takriban, katika taifa zima. Kwa zaidi ya miaka ishirini, sehemu kubwa ya nchi ilishindwa kushiriki kwenye upigaji kura kwa sababu ya uhasama ulioshtadi wakati huo baina ya maeneo ya kaskazini na kusini, mapigano yaliosababisha vifo vya watu milioni 2, na ambapo raia milioni 4 waling’olewa makazi, na watu 600,000 walivuka mipaka kuelekea mataifa jirani kutafuta hifadhi. Tukio la kuitisha uchaguzi ni moja ya suala muhimu linaloambatana na Mapatano ya Amani ya Jumla ya 2005, na ni hatua iliosaidia kusitisha mapigano baina ya Sudan kaskazini na kusini.