Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali ya kijamii kwa watoto na wanawake Zimbabwe ni mbaya, inasema UM

Hali ya kijamii kwa watoto na wanawake Zimbabwe ni mbaya, inasema UM

Shirika la UM juu ya Mfuko wa Maendeleo kwa Watoto (UNICEF) likijumuika na Serikali ya Zimbabwe leo limetangaza takwimu mpya za maendeleo ya jamii, takwimu zenye kuonyesha hali ya wanawake na watoto wadogo katika Zimbabwe inaendelea kuharibika na kuwa mbaya zaidi.

Kiashirio cha Jumla na Uchunguzi wa Kufuatilia (MIMS), kilitumiwa kuenedeleza uchunguzi wa maendeleo ya kijamii mnamo mwezi Mei 2009, na kilithibitisha wanawake na watoto wadogo walinyimwa fursa za kupatiwa huduma muhimu za kimaisha, hasa wale wakazi maskini wa katika vijiji. Kwa mujibu wa Dktr. Peter Salama, Mwakilishi wa UNICEF Zimbabwe, watoto 100 chini ya umri wa miaka mitano huwa wanakadiriwa kufariki kila siku katika Zimbabwe kutokana na magonjwa yanayozuilika. Vile vile watoto hufariki kwa sababu ya kupatwa na VVU/UKIMWI, matatizo yanayotokana na uzazi dhaifu, homa ya vichomi na kuharisha. Takwimu pia zimegundua tatizo la kushtusha ambapo ilionekana kwamba katika Zimbabwe ya leo miongoni mwa kila mama wawili wajawazito, mmoja wao hujifungua majumbani bila ya uangalizi wa wahudumia afya, kwa sababu ya ukosefu wa fedha za matibabu.