Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Aliyekuwa ofisa wa upelelezi Rwanda kukana mashtaka ya Mahakama ya ICTR

Aliyekuwa ofisa wa upelelezi Rwanda kukana mashtaka ya Mahakama ya ICTR

Idelphonse NIZEYIMANA, aliyekuwa ofisa wa idara ya upelelezi katika Rwanda, amekana makosa ya kushiriki kwenye mauaji ya halaiki pale alipohudhuria Ijumatano Mahakama ya Kimataifa juu ya Rwanda (ICTR), kuandikisha jibu la kesi alioshtakiwa na mahakama hiyo.

Nizeyimana alishikwa tarehe 05 Oktoba mjini Kampala, Uganda baada ya kukimbia huku na kule kwa miaka tisa kukwepa mashitaka. Kufuatia kushikwa kwake Nizeyimana alihamishiwa kituo cha kuweka watu kizuizini cha Mahakama ya ICTR kilichopo Arusha, Tanzania. Nizeyimana anakabiliwa na mashitaka matano yanayohusu mauaji ya halaiki, uchochezi wa kuendeleza mauaji ya kuangamiza kabila, pamoja na makosa ya jinai dhidi ya utu yaliofanyika dhidi ya raia wa KiTutsi wanaokadiriwa 800,000, pamoja na wazalendo wennziwao wa KiHutu, wenye siasa ya wastani walipouliwa kihorera na Wahutu katika 1994, kwa kutumia zaidi mapanga, katika kipindi cha chini ya siku mia moja. Miongoni mwa makosa aliyoshtakiwa Nizeyimana kuyatenda hujumuisha lile kosa la kuhukumu kuuliwa aliyekuwa Malkia wa Rwanda, Rosalie Gicanda ambaye aliwakilisha uzalendo halisi wa Watutsi. Tarehe ya kesi ya mtuhumiwa Nizeyimana inatarajiwa kutangazwa na mahakama katika siku za baadaye.