Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNAIDS inashauriana na mashirika ya kikanda kudhibiti UKIMWI Afrika ya Kati/Magharibi

UNAIDS inashauriana na mashirika ya kikanda kudhibiti UKIMWI Afrika ya Kati/Magharibi

Majuzi katika mji wa Dakar, Senegal kulifanyika kikao maalumu cha ushauriano, kilichoandaliwa na Jumuiya ya Mashirika ya UM dhidi ya UKIMWI (UNAIDS) pamoja na jumuiya 30 za kiraia, kwa lengo la kubuni miradi itakayohakikisha umma huwa unapatiwa uwezo wa kujikinga na UKIMWI, na kupata huduma zinazoridhisha za matibabu, pamoja na uangalizi na misaada ya fedha inayohitajika kutekeleza huduma hizo za afya kwa waathirika.

Washiriki wa mkutano walisema vizingiti kadha wa kadha bado vimesalia na wadau wote husika wanahitajika kukabiliana navyo kwa haraka, ili kuuwezesha umma wa Afrika Magharibi na Afrika ya Kati kupata fursa ya kuhudumiwa afya kinga dhidi ya maambukizi maututi ya UKIMWI, pakihatajika. Wajumbe walioshiriki kwenye kikao hicho cha mashauriano walipendekeza mambo sita ambayo waliamaini ni muhimu kuzingatiwa kuustiri umma wa eneo lao na UKIMWI: walitaka kuwepo mfuko maalum, wa kusarifika, utakaotumiwa kukabiliana na majukumu ya kudhibiti UKIMWI; walitaka huduma za kijinsiya na afya ya uzazi kuwa zinafungamanishwa na tiba ya maradhi ya UKIMWI na kifua kikuu; walipendekeza mfumo wa kijamii na kisheria huwa unaendelezwa vizuri zaidi; na kuhakikisha watu huwa na uwezo wa kupata matibabu, na wakati huo huo kuharakisha huduma kinga kwa umma; vile vile walitaka kuhakikisha mama wajawazito huwa na fursa ya kupatiwa dawa kinga za kuhifadhi watoto na maambukizi ya VVU; na kulikubaliwa kuongeza jitihadi za kuwa na ushirikiano unaofaa wa kikanda, miongoni mwa wadau wote husika, pamoja na kuwa na mawasiliano yanayoridhisha miongoni mwao.