Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kamishna wa Haki za Binadamu ameshtushwa na idadi ya majeruhi na maututi katika Xinjiang

Kamishna wa Haki za Binadamu ameshtushwa na idadi ya majeruhi na maututi katika Xinjiang

Navi Pillay, Kamishna Mkuu wa UM juu ya Haki za Binadamu amenakiliwa Ijumanne akieleza kuwa ameshtushwa sana na idadi kubwa ya majeruhi na mauaji yaliotukia mwisho wa wiki iliopita, kutokana na fujo zilizofumka katika eneo la Urumqi, mji mkuu wa Jimbo la Uchina Linalojitawala la Xinjiang.

Taarifa zilizotolewa Ijumatatu na Serikali zilieleza watu 150 ziada waliuawa na watu 800 wengine walijeruhiwa, kufuatia mapambano yaliotukia Ijumapili iliopita baina ya makabila yanayohasimiana katika Xinjiang.  Pillay alisema idadi ya vifo na majeruhi ni "kubwa sana kwenye mazingira ya vurugu lisiochukua hata siku moja!" Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu aliwakumbusha wenye mamlaka wa jimbo la Xinjiang kwamba ni wajibu wao kuhakikisha umma una haki ya uhuru wa kusema, haki inayotekelezwa kwa amani, inayohishimiwa na kudumishwa kwa uwiano na sheria za kimataifa. Kadhalika, alisisitiza, wenye mamlaka pia wanawajibika kuhakikisha sheria na utulivu wa raia unadumishwa, na walitakiwa wajiepushe na matumizi ya nguvu, yanayoweza kuua, ili kama imehakikishwa hali ni isioepukika na maisha ya raia ni lazima yahifadhiwe kwa kuchukua hatua hiyo. Pillay aliwasihi viongozi wa kiraia wa makabila ya Uighur na wale wa makabila ya Kichina ya Han, pamoja na wenye madaraka, kwa ujumla, kutoka viwango vyote vya utawala, kujitahidi kama wawezavyo "kuonyesha uvumilivu mkubwa miongoni mwao na kujizuia na tabia ya kuchochea mambo, hali ambayo huenda ikazusha na kupalilia vurugu, na mauaji ya raia wasio hatia."