Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Utawala na uthabiti unaanza kurudi Somalia asema Mjumbe Maalum wa UM

Utawala na uthabiti unaanza kurudi Somalia asema Mjumbe Maalum wa UM

Akiliarifu Baraza la Usalama juu ya hatua za kuchukuliwa katika kutekeleza makubaliano ya Djibuti, huko Somalia, Mjumbe Maalum wa UM amesema utawala wa kisheria umeanza kurudi huko Mogadishu, kukiwepo na serekali na taasisi za utawala zinazo tambuliwa kikanda, kimataifa na idadi kubwa ya wa-Somali.

Bw Ahmedou Ould-Abdallah amesema, kutokana na nia hii ya dhati ya kurudisha amani na utulivu katika taifa hilo, jumuia ya kimataifa inabidi kuchukua hatua za haraka kusaidia utawala mpya, kutoa msaada haraka wa kidiplomasia na kifedha kwa kikosi cha kulinda amani AMISON, kuwasilisha bila ya kipingamizi chechote cha huduma za dharura, na kusaidia kukarabati taasisi za usalama na mahakama ya Somalia. Mjumbe Maalum alipongeza juhudi za mataifa jirani, UM, AU, Umoja wa nchi za Kiarabu, Umoja wa Ulaya kila mtu aliyesaidia kufikia hatua hii muhimu kabisa ya kurudisha utulivu katika taifa hili la pembe ya Afrika, lenye utajiri mkubwa kwenye ufukwe wake wa bahari. Waziri wa mambo ya nchi za njee wa Somalia, Mohamed Abdullahi Omar akizungumza kwa mara ya kwanza mbele ya baraza hilo amesema, nchi yake hivi sasa haishikwa mateka na mababe wa kivita, vita vya kikoo, wala makundi ya kisiasa. Amesema Somalia iko njiani kurudi kua taifa lenye utawala wa kisheria inayohitaji msaada kamili wa jumuia ya kimataifa kudumisha amani na utulivu pamoja na maendeleo, kwa njia majadiliano bila ya mtutu wa bunduki.