Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wataalamu watathminia umadhubuti wa miradi ya kufyeka rushwa Afrika

Wataalamu watathminia umadhubuti wa miradi ya kufyeka rushwa Afrika

Wataalamu wanaohusika na udhibiti wa ulajirushwa, kutoka mataifa kadha ya Afrika, wamekamilisha mkutano wa siku mbili uliofanyika Kigali, Rwanda ambapo kulitathminia umadhubuti na athari za taasisi za Kupiga Vita Ulajirushwa barani Afrika.

 Mkutano uliotayarishwa bia na Kamisheni ya UM juu ya Uchumi wa Afrika (UNECA) pamoja na Shirika la Miradi ya Maendeleo (UNDP), ulikusudiwa hasa kufanya utafiti kamili juu ya vyanzo na athari za vitendo vya ulajirushwa, kwa kuambatana na mazingira ya kiuchumi na jamii yaliopo Afrika. Kwa mujibu wa matokeo ya uchunguzi ulioendelezwa na Kamisheni ya UNECA, yameonyesha bara la Afrika ndio eneo ambalo bado liko nyuma sana katika kupambana na matatizo yaliopamba ya ulajirushwa na milungura. Kadhalika utafiti uliofanywa kipamoja na Benku Kuu ya Dunia, UNDP na Jumuiya ya Kimataifa kuhusu Uangavu wa Majukumu imethibitisha Afrika haikufanikiwa, kama inavyopaswa, kukabiliana na ‘uovu' wa rushwa, hususan kwenye serikali na katika shughuli za utawala.