Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hapa na pale

Hapa na pale

Ijumatano, KM Mdogo na Mshauri wa UM juu ya Misaada ya Daharura, John Holmes alikamilisha ziara ya siku tatu Ethiopia. Ijumanne, Holmes alizuru eneo la wenyeji wa asli ya Kisomali, sehemu ya nchi iliodhurika sana na ukame, pamoja na bei kubwa ya chakula na mgogoro unaozidi kuendelea katika eneo lao. Kwenye kituo cha ukaguzi juu ya hadhi za wahamiaji, Holmes akikutana na wenyeji raia wa Kisomali na Kiethiopia waliokata tama ya maisha na ambao walitaka kusaidiwa kihali, halan. Alikumbusha Holmes ya kuwa ukosefu wa misaada ya kiutu umewalazimisha wahamiaji wingi wa Kiethiopia kutafuta hifadhi ya kisiasa, kwa matumaini ya kupatiwa chakula, makazi na huduma za afya.

Demetris Christofias, Kiongozi wa Magiriki wa Cyprus pamoja na Kiongozi wa Waturuki wa Cyprus, Mehmet Ali Talat, leo walikutana kuanzisha majadiliano rasmi yenye lengo la kuwasilisha suluhu ya jumla kwenye suala sugu la Cyprus. KM aliyapongeza mazungumzo hayo, kwenye risala alioituma mkutanoni ambayo ilisomwa na Mshauri Maalumu wa UM kwa Cyprus, Alexander Downer na aliyakaribisha majadiliano na kuunga mkono kidhati mchango wa viongozi wa jamii zote mbili za Cyprus – yaani jamii za Kigiriki na Kiturki – na ushirikiano wao ulioonyesha uzito mkuu na maelewano, hasa kwa ahadi yao kwamba wamewania kuhakikisha mpango wa amani utakamilishwa kwa mafanikio.

Shughuli za kuwatafuta abiria walionusurika na ajali ya ndege ilioanguka nje ya Bukavu, katika JKK bado zinaendelea, saa 48 baada ya ajali hiyo kujiri. Kutokana na taarifa za awali juu ya uchunguzi ilofanyika wa anga, mabaki ya ndege yameonyesha kulikuwepo mgongano wa nguvu wa ndege, na hakuna dalili abiria waliweza kusalimika. Timu ya utafutaji huo inajumlisha vikosi vya Shirika la UM juu ya Ulinzi wa Amani katika JKK (MONUC), watumishi wa Idara ya Vyombo vya Anga vya Kiraia Kongo, pamoja na mshauri wa operesheni za ndege ya AirServe, kampuni yenye kumiliki ndege ilyoanguka, pamoja na Timu Maalumu ya Uokoaji ya Afrika Kusini. Timu zote hizi zimechanganyisha operesheni zao za anga na ardhini ili kuhakikisha kila ncha ya eneo la ajali inakaguliwa kwa makini zaidi.

Ripoti kutoka Vikosi vya Mchanganyiko vya UM/UA kwa Darfur (UNAMID) inayosema kumegunduliwa kukithiri kwa idadi ya Polisi wa Serikali ya Sudan karibu na kambi ya wahamiaji wa ndani ya Kalma iliopo Nyala. Kwa mujibu wa UNAMID, doria ilioendelezwa na UNAMID Ijumatatu katika Nyala ilishuhudia kuongezeka kwa polisi, amnbao walikutikana wakiegesha mahema mengi kwenye eneo jipya liliopo kilomita tano karibu na kambi ya wahamiaji. Kwa hivyo UNAMID imeamua kueneza vikosi vya pamoja vya kudumu vya wanajeshi na polisi, halkadhalika, kwenye eneo hilo. Vile vile polisi wa UNAMID watakuwa na watu wao, kwa saa 12 kila siku, ndani na karibu ya kambi ya Kalma. Tangu tarehe 25 Agosti UNAMID imeongeza doria za vikosi vyake katika eneo hilo la Darfur.