Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hifadhi ya muda ya wageni wakaazi huenda ikasitishwa Afrika Kusini

Hifadhi ya muda ya wageni wakaazi huenda ikasitishwa Afrika Kusini

Ripoti ya awali wiki hii itasailia hali ya wageni Afrika Kusini, ambao mnamo miezi miwili iliopita waliathirika na vurugu liliofumka nchini humo dhidi yao. Tutalenga ripoti juu ya hifadhi ya muda ya makazi kwa wahamiaji hawo katika jimbo la Gauteng.~

Mmoja wa raia wa Zimbabwe, anayetafuta hifadhi ya kisiasa Afrika Kusini, ambaye tutatumia jina la kupanga kwa usalama wake, na tutamwita Gloria, ni miongoni mwa umma mwathiriwa atakayelazimika kutafuta makazi mengine ya muda kujishikiza kimaisha, kufuatia kufungwa kwa mastakimu ya serikali ya Gauteng. Kwa mujibu wa ripoti za UNHCR wakati Gloria alipokuwa kwao Zimbabwe aliishi maisha ya anasa kwa sababu mumewe, aliyemaliza shahada mbili za chuo kikuu, alikuwa na kazi nzuri ya. Lakini maisha ya Gloria yalibiruliwa, na kuwa songo mbingo, baada ya mumewe kuuawa katika 2005 kwa sababu alikuwa mawanaharakati wa chama cha upinzani cha Vuguvugu la Mageuzi ya Kidemokrasia (MDC).

Ofisi ya UNHCR iliopo Pretoria, ikijumuika na Shirika la Huduma za Wahamiaji la Wajesuti (JRS), inajitahidi kuwasaidia wahamiaji wote waliomba hifadhi ya kisiasa kutoka Serikalini, kama Gloria, pamoja na Wazimbabwe waliokosa vitambulisho vya ukaazi Afrika Kusini na kutaka waunganishwe na jamii za kienyeji ili waweze kujihudumia kimaisha.

Gloria, alisema anaelewa hali ya dharura iliopo kuhusu makazi ya muda kwa wahamiaji, na anaishukuru UNHCR kwa mchango wake wa kuwasaidia wahamiaji kama yeye kusahilisha masaibu yaliyowazonga kimaisha ugenini. Lakini pia, alitilia mkazo Gloria, wakati umewadia wa kusonga mbele kimaisha na angelipendelea apatiwe muda zaidi kidogo wa kujitayarisha kutekeleza mipango yake hiyo katika Afrika Kusini.