Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Suala la kukomesha silaha ndogo ndogo Afrika ya Kati linaongoza ajenda ya mazungumzo ya UM

Suala la kukomesha silaha ndogo ndogo Afrika ya Kati linaongoza ajenda ya mazungumzo ya UM

Kamati ya Ushauri ya UM juu ya Masuala ya Usalama wa Afrika ya Kati, inayokutana wiki hii katika kikao cha mawaziri mjini Yaounde, Cameroon imezingatia hatua za kuchukuliwa kipamoja kudhibiti bora tatizo la silaha ndogo ndogo na silaha nyepesi kieneo. Kadhalika Kamati ilizingatia uwezekano wa kurekibisha kanuni zao na kubuni sheria mpya za kuongoza shughuli za vikosi vya usalama kwenye maeneo husika.

Kadhalika ulisailia maendeleo yaliojiri karibuni kwenye shughuli za usalama, ikichanganyika na mabadiliko ya kisiasa miongoni mwa mataifa wanachama. Kamati ya Ushauri juu ya Usalama wa Afrika ya Kati, ambayo ilibuniwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa mwezi Mei 1992, hukutana mara mbili kila mwaka. Kamati hii inajumuisha wajumbe kutoka Angola, Burundi, Cameroon, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad, Jamhuri ya Kongo, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na pia Guinea ya Ikweta, Gabon, Rwanda na Sao Tome na Principe.