Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Biashara za vijijini Afrika zitafaidika na mfuko mpya wa UM

Biashara za vijijini Afrika zitafaidika na mfuko mpya wa UM

Shirika la UM juu ya Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) lilitangaza majuzi mjini Cape Town, Afrika Kusini kwenye mkutano wa Athari za Uchumi wa Dunia kwa Afrika, ya kwamba litaanzisha taasisi mpya ya mfuko wa maendeleo kusaidia wanavijiji masikini katika Afrika, kupata fedha za kuanzisha aina mpya ya biashara kwenye maeneo yao.

Mfuko huu unajulikana kama Mfuko wa Kukabiliana na Shughuli za Biashara kwa Afrika au Mfuko wa AECF, taasisi ambayo ipo tayari kufadhilia kila mradi wa maendeleo ya vijijini msaada wa fedha unaofika hadi dola milioni moja na nusu. Mfuko wa AECF unatazamiwa kushughulikia huduma hizo kwa muda wa miaka saba kuanzia 2008. Hivi sasa Mfuko wa AECF umeshapokea mchango maridhawa wa fedha wenye uwezo wa kuanzisha operesheni zake, halan, mchango ambao ulijumuishwa na Shirika la IFAD, Benki ya Maendeleo Afrika (ADB), Jumuiya ya Ushauri Kusaidia Masikini pamoja na serekali za Uingereza na Uholanzi.

Msaada huu ukitekelezwa unatarajiwa kuleta natija kubwa za kiuchumi kwa wanavijiji masikini wanaoishi katika bara la Afrika, hasa ilivyokuwa katika kila watu masikini 10 wanaoishi kwenye bara hilo 7 yao hufanya mastakimu yao kwenye maeneo yaliopo mbali na miji.