Samaki mkunje angali mbichi. Hapa ni fukwe ya Watamu nchini Kenya wanafunzi wakielimishwa jinsi ya kusafisha fukwe na kuhifadhi viumbe vya baharini. Baada ya elimu wanamuona kasa na kumrejesha taratibu baharini kwani uhai wa viumbe vya bahari ni uhai wa binadamu na sayari ya dunia.
Utunzaji wa miche ya miti aina ya Mukau. Miti hii ya asili pamoja na kuleta kivuli, majani yake makavu kurutubisha ardhi na umande wake kuimarisha mazao yaliyo ardhini ni chanzo pia cha kipato kwa wanaoipanda. Mauzo ya mbao ya miti ya Mukau iliyopandwa katika eka moja ni dola 29,000.
Nchini Msumbiji baada ya vimbunga Idai na Kenneth kuezua paa za nyumba, sasa UN-Habitat imekuja na mradi wa ujenzi wa nyumba ambazo boriti za paa la nyumba zinakuwa imara zaidi na paa halichomozi nje ya nyumba. Kwa hiyo upepo haupati mahali pa kujikinga na kuezua paa.
"Ngoja ngoja huumiza matumbo" methali hii imethibitishwa na vijana hawa baada ya kuona viongozi hawachukua hatua za kutosha dhidi ya mabadiliko ya tabianchi waliandamana huko Karua, Nairobi nchini Kenya wakidai hatua zaidi kwani kesho yao iko mashakani iwapo madhara ya sasa dhidi ya sayari dunia yataendelea.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa inasema magari kuukuu ni sababu ya ongezeko la hewa chafuzi na hali inakuwa mbaya zaidi pale wanunuzi wa magari wanapobadili mfumo wa injini na kuondoa kifaa cha kuzuia hewa chafuzi, "catalytic converter" kama katika gari hili la abiria, maarufu kama Matatu jijini Nairobi, Kenya.
Nchini Tanzania mbinu bora za kilimo kinachohimili mabadiliko ya tabianchi zinazotolewa na shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO kwa wakulima mkoani Kigoma zimezaa matunda baada ya wakulima wa wilayani Kakonko kuvuna zao la muhogo walilopanda kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu
Idadi kubwa ya wakulima nchini Bangladesh sasa wanapanda aina mpya ya mazao kama vile mpunga ulioboreshwa kwa teknolojia ya nyuklia kwa ushirikiano na shirika la Umoja wa Mataifa la nishati ya atomiki, IAEA. Mpunga huo unakomaa kwa muda mfupi, unastahimili udongo wenye chumvi na mavuno ni mengi.