Tamu ya uhuru haikudumu! Mwezi Desemba mwaka 2013 mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yalizuka nchini Sudan Kusini. Raia walilazimika kukimbia makazi yao na kusaka hifadhi maeneo mbali mbali. Kuna waliokimbilia nchi jirani ikiwemo Uganda huku wengine wakikimbilia katika vituo vya ulinzi wa raia vinavyolindwa na ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS mjini Juba. Pichani wananchi wakiwa wamejificha kukwepa mashambulizi.
Chungu iliendelea. Vikundi vilivyojihami pamoja na vikosi vinavyopingana na serikali ya Sudan Kusini viliripotiwa kukamata watoto na kuwatumikisha jeshini. Watoto walitumika kwenye mapigano na pia kama silaha ya vita na hivyo utoto wao kugubikwa na machungu na kukoseshwa haki zao za msingi za kuishi, kuendelezwa, kulindwa na kushirikishwa.
Katika picha hii ya mwaka 2014, watoto wanaonekana wanatembea katika eneo lililofurika kwenye kituo cha kuhifadhi raia, huko Bentiu, kituo kilichokuwa chini ya Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani Sudan Kusini, UNMISS. Kituo kilikuwa na watu zaidi ya 40,000 na kilikuwa kimbilio la raia wakati wa mapigano yaliyoanza Desemba 2013. Kila msimu wa mvua, mafuriko ndio pahala pake. Lakini UNMISS ilikuwa inachukua hatua kila wakati kuhakikisha mazingira yanakuwa bora.
Utapiamlo ni changamoto kubwa kwa watoto nchini Sudan Kusini. Pichani kushoto ni Nyamilow Nangdor, mama wa watoto wanne akiwa na mfanyakazi wa kujitolea wa masuala ya lishe Fatai Deng kwenye moja ya mashamba darasa ya kilimo cha mboga za majani huko Bentiu. Bustani hii inaendeshwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF ikiungwa mkono na shirika la kiraia la afya ya jamii na maendeleo, CHADO. Mradi huu unatekelezwa Bentiu na Rubkona kwa lengo la kufundisha akina mama 30,000 ambao watoto wao wana utapiamlo.
Maji nayo ni tatizo kubwa kwa wakazi wengi wa Sudan Kusini. Kwa kutambua hilo, UNICEF imejenga mtambo wa kusukuma maji unaotumia nishati ya jua huko Yambio. Mtambo unasukuma maji kwenda maeneo ya vilimani kwa ajili ya jamii, shule na vituo vya afya. Nishati ya jua ni nzuri na ni nafuu katika kuhakikisha jamii maskini na zilizo maeneo ya ndani zaidi zinapata umeme kwa kuwa mara nyingi hazifikiwi na umeme wa gridi ya taifa. Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, Sudan Kusini ina mkwamo mkubwa katika kupata huduma ya umeme na hivyo nishati ya sola haihitaji vifaa vingi na vya gharama kubwa.
Ni sawa na kuua ndege wawili kwa jiwe moja. Hapa ni kituo cha lishe, kuna eneo la michezo kwa watoto wakitumia wanasesere walionunuliwa na wa kutengenezwa hapa kwa kutumia vitu kama vile kamba za minazi. Mafunzo haya yanalenga kujengea uwezo mama na mtoto kujitengenezea wanasesere wao. kwa kucheza , ubongo wa mtoto unachechemuliwa na ni muhimu kwa maendeleo ya baadaye hasa anapokuwa amepona utapiamlo. UNICEF imeanzisha mbinu hii ya makuzi ya mapema ya mtoto kupitia mradi wa boresha lishe Sudan Kusini.
Mwaka jana kutangazwa kwa janga la ugonjwa wa Corona au COVID-19, ilikuwa pigo pia kwa Sudan Kusini. Shule zilifungwa. Hata hivyo hatua zilichukuliwa na masomo yakaendelea kwa nija ya redio kama inavyoonekana pichani, Angures Buba [kulia) yuko darasa la 8 na Christine Poni (kushoto) darasa la 6 wanasomea nyumbani. Angres anasema "nakumbuka sana shule. Nakumbuka walimu. Si rahisi kila mara kuelewa kile mwalimu anafundisha kwa njiaya redio."
Mustakabali wa Sudan Kusini unategemea vile ambavyo watoto wa nchi hiyo watakuzwa katika mazingira gani. Ndio maana shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF linahaha watoto wapatiwe haki zao za msingi. Ujenzi wa vituo vya lishe vimekuwa nuru kwa mtoto Bathi (pichani) akiwa amebebwa na mama yake Nyachimach. Tabasamu la Bath linatia matumaini.