Afrika Kusini ina jumla ya walinda Amani 1,260 kwenye operesheni mbalimbali za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa ambapo kati yao hao wanawake ni 191 na wanaume ni 1,069. Azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linasihi ushiriki sawia wa wanawake na wanaume kwenye operesheni zote za ulinzi wa amani ikiwemo kwenye jeshi.
Katika doria hizi walinda amani hawa wanawake wanasaidia kujenga Imani miongoni mwa raia na hivyo kufanikisha shughuli za maendeleo ikiwemo kilimo. Walinda amani wanawake siyo tu wanafanya kazi kama wafanyazo wanaume ikiwemo kuongoza vikosi hadi kwenye uwanja wa mapambano, bali pia wanaongeza thamani kwenye operesheni za kijeshi ikiwemo kutoa maamuzi kuhusu masuala yanayogusa raia hasa wanawake na wasichana.
Mlinda amani mwanamke katika ujumbe wa MONUSCO huko DRC akiwa lindoni kwenye nchi hiyo ambayo machafuko yameshamiri hasa maeneo ya mashariki mwa nchi. Umoja wa Mataifa unasema kupelekwa kwa walinda amani wanawake kwenye maeneo yenye mizozo huchangia amani endelevu kwa kuwa hujenga imani na ustawi miongoni mwa wanawake na wasichana walioko kwenye maeneo ya mizozo.
Baadhi ya stadi za kipekee ambazo walinda amani wanawake wanachangia kwenye ulinzi wa amani ni pamoja na ukaguzi wa raia wanawake, kukagua majumba na maeneo ambako kitamaduni si sawa kwa wanaume kufanya upekuzi. Jamii kwenye nchi ambako operesheni za ulinzi wa amani zinafanyika hujisikia vyema zaidi pindi wanaposhirikiana na operesheni zenye mchanganyiko wa wanawake na wanaume. Kama ilivyo pichani huko Beni.
Walinda amani hawa wanawake kutoka Afrika Kusini wakiwa kwenye doria yao huko Kivu Kaskazini wanaendesha doria ambazo kwazo hujenga imani kwa wananchi. Jimbo la Kivu Kaskazini linakuwa na machafuko mara kwa mara ambako vikundi vilivyojihami hushambulia raia na hata kusababisha vifo.
Doria pia hufanywa kwa miguu, ambapo walinda amani hawa wa kikosi cha askari wanawake kutoka Afrika Kusini wanaohudumu kwenye kikosi cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa, DRC, MONUSCO husaidia kusongesha mbele azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la kutaka ujumuishaji zaidi wa wanawake kwenye operesheni za ulinzi wa amani ili kuchagiza amani endelevu kwenye maeneo ya mizozo.