Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNGA80

Mkutano wa Baraza Kuu - Taarifa Maalum ya UNGA80
23 Septemba – 30 Septemba 2025
Jukwaa limewekwa tayari kwa ajili ya Mjadala Mkuu wa Mkutano wa 80 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Mkutano huu utafunguliwa chini ya kaulimbiu “Bora Pamoja: Miaka 80 na Zaidi kwa Amani, Maendeleo na Haki za Binadamu”, ikiwa ni hatua muhimu inayofanyika katikati ya changamoto kubwa duniani na wito wa dharura wa kuchukua hatua mpya za ushirikiano wa kimataifa.
Mjadala wa Ngazi ya Juu utaanza rasmi tarehe 22 Septemba kwa siku nzima ya mikutano ya kilele na maadhimisho, ikiwemo kumbukumbu ya miaka 80 tangu kuanzishwa kwa Umoja wa Mataifa, tukio la wakati wa Malengo ya Maendeleo Endelevu au SDG Moment na kutimia miaka 30 tangu Mkutano wa Dunia wa Beijing kuhusu wanawake. Viongozi pia watashiriki kwenye mkutano wa ngazi ya juu kuhusu Suluhu ya amani kwa suala la Palestina na utekelezaji wa suluhu ya mataifa mawili.
Kuanzia tarehe 23 hadi 29 Septemba, macho na masikio ya dunia yatageukia jukwaa maarufu lenye marumaru ya kijani ndani ya Ukumbi wa Baraza Kuu, ambapo marais, mawaziri wakuu na wafalme watawasilisha taarifa za kitaifa, wakibainisha dira zao kuhusu amani, maendeleo, haki za binadamu na hatua za pamoja wakati huu wa changamoto zinazoongezeka duniani.
Ajenda pia itahusisha mkutano wa kilele unaofanyika kila baada ya miaka miwili kuhusu ufadhili wa maendeleo endelevu, Mkutano wa Tabianchi, uzinduzi wa Mazungumzo ya kimataifa kuhusu Usimamizi wa Akili Mnemba AI, Hatua za dunia kuhusu magonjwa yasiyoambukiza NDCs na afya ya akili, pamoja na hali ya Waislamu Warohingya na wengine walio wachache nchini Myanmar.
Hapa, Idhaa ya Kiswahili inakupa fursa ya kuketi mstari wa mbele kushuhudia yote yanayojiri. Kupitia simu yako ya rununu au kompyuta, fuatilia Wakuu wa Nchi na Serikali wanapojadili masuala makubwa ya wakati wetu na kuelekeza dira ya taswira mpya ya Umoja wa Mataifa.
 
Tembelea majukwaa yetu ya mitandao ya kijamii: Youtube: Habari za UN X: Habari za UN
Mtazamo mpana wa mkutano wa ngazi ya juu wa Baraza Kuu la kuadhimisha miaka themanini ya kuanzishwa kwa Umoja wa Mataifa.
UN Photo/Loey Felipe

Umoja wa Mataifa waadhimisha miaka 80 tangu kuanzishwa kwake

Umoja wa Mataifa hii leo umeadhimisha miaka 80 tangu kusainiwa kwa Mkataba wake tarehe 26 Juni 1945, tukio lililotoa matumaini mapya kwa dunia iliyokuwa imechoka kutokana na vita kuu mbili za dunia, mauaji ya halaiki na ukoloni. Katika maadhimisho hayo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amesema kumbukizi ya kuanzishwa kwa Umoja wa Mataifa ni fursa ya kukumbuka ujasiri wa waanzilishi wa taasisi hiyo na kuimarisha mshikamano wa kimataifa katika kukabili changamoto zinazokabili dunia hivi sasa. 

Sauti
4'8"
Emily Mohohlo, Mratibu wa shirika la kiraia la Slum Dwellers International kutoka Afrika Kusini, akizungumza na Assumpta Massoi kandni mwa mkutano wa UNGA80 mjini New York Marekani.
UN News

Tumefika hapa UN, tafadhali tusikilizeni

Kando ya maadhimisho ya siku ya miaka 80 ya Umoja wa Mataifa, hapa makao makuu kumefanyika mashauriano ya faragha yenye lengo la kusaka majawabu ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Mashauriano ya leo ni sehemu ya mashauriano 10 yatakayofanyika kuelekea mkutano wa tabianchi wa wakuu wa nchi na serikali utakaofanyika keshokutwa Jumatano hapa Umoja wa Mataifa. 

Sauti
2'22"