Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Maambukizi ya ukimwi kwa watoto kutokomezwa: Viongozi wa Afrika /UNAIDS

Maambukizi ya ukimwi kwa watoto kutokomezwa: Viongozi wa Afrika /UNAIDS

Pakua

Mawaziri wa afya na wawakilishi kutoka nchi 12 za Afrika na wadau wa kimataifa leo wameahidi na kuweka mipango ya kutokomeza ukimwi miongoni mwa watoto ifikapo mwaka 2030,  limesema shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na kutokomeza VVU na ukimwi UNAIDS.

Ahadi hiyo imetolea jijini Dar es salaam Tanzania wakati wa uzinduzi wa “Muungano wa kimataifa kutokomeza ukimwi kwa wtoto Afrika” muungano ambao utafanyakazi kwa miaka 8 hadi mwaka 2030 ukilenga kushughulikia moja ya changamoto kubwa katika vita dhidi ya ukimwi. 

Taarifa ya UNAIDS inasema wakati robo tatu ya watu wazima wanaoishi na virusi vya ukimwi VVU wako katika matibabu au asilimia 76% , Watoto ni nusu tu sawa na asilimia 52% ndio wanaopata matibabu ya dawa za kurefusha maisha na kupunguza makali ya ukimwi.  

Na kwa mujibu wa takwimu za shirika hilo mwaka 2021 jumla ya watoto 160,000 walipata maambukizi mapya ya VVU na watoto ni asilimia 15% ya vifo vyote vitokanavyo na ukimwi licha ya kwamba wao ni asilimia 4% pekee ya watu wote wanaoishi na VVU.  

Kwani hivi sasa kote duniani mtoto hufa kila baada ya dakika 5 kutokana na sababu zinazohusiana na ukimwi. 

Muungano huo mpya “ni wa kutetea na kuhamasisha dhamira ya kisiasa na rasilimali ili kuhakikisha hatua na uwajibikaji kuhusu malengo na ahadi za pamoja.” 

Katika awamu hii ya kwanza nchi 12 zimejiunga na muungano huo ambazo ni  

Angola, Cameroon, Côte d'Ivoire, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, Kenya, Msumbiji, Nigeria, Afrika Kusini, Tanzania, Uganda, Zambia,na Zimbabwe.  

Tanzania ambayo ni mwenyeji wa mkutano wa uzinduzi wa muungano huo uliofanyika jijini Dar es salaam imekuwa ya kwanza kujisajili.  

Audio Credit
Flora Nducha
Audio Duration
1'59"
Photo Credit
© UNICEF/Karin Schermbrucker