Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Japo tupo kambini lakini mkopo wa UNICEF umetukomboa kiuchumi

Japo tupo kambini lakini mkopo wa UNICEF umetukomboa kiuchumi

Kutokana na mabadiliko ya mifumo ya mvua, hali ambayo imekuwa ikileta maafa nchini Burundi na kusababisha mafuriko, maporomoko ya ardhi na kuharibu mazao, Jeannette Niyibigira, pamoja na mumewe na watoto 5, walilazimika kuyahama makazi yao ya Gatumba, na sasa wanaishi katika kambi ya Kiragaramango ambako kama si mkopo mdogo kutoka shirika la Foi En Action (Faith in Action) ambalo ni wadau wa UNICEF, Camp, maisha yangekuwa magumu zaidi. Taarifa ya Lucy Igogo inaeleza zaidi. 

 

Ni Jeannette Niyibigira, mama wa watoto watano na yatima mmoja ambaye anamlea. Mama huyu anasema, "tulikuwa na hofu. Kulikuwa na maji kila mahali. Tulikuwa tunajaribu kuokoa watoto wakati maji yalikuwa yakijaza nyumba yetu na kuchukua kila kitu tulichomiliki. Hatukuwa na chochote kilichobaki, hakuna kitu cha kula, tulikuwa tumepoteza kila kitu." 

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto na mdau wake Faith in Action waliingilia kati na kumfanya mama huyu aweze kujimudu tena pale walipompatia mkopo kama anavyoeleza akisema, "tunaishi na mume wangu katika eneo la Kigaramango. Walinipa mkopo wa pesa za kutengeneza cherehani yangu ambayo iliharibiwa na maji ili nianze kushona tena. Wakati mwingi mimi hufanya kazi saa 6 hadi 7 kwa siku. Ninapata fedha faranga 8 hadi 10,000 za Burundi kwa siku sawa na dola 4 hadi 5 za kimarekani. Kile ninachopata kiliniruhusu kurudisha watoto darasani na ninaweza kuwapatia chakula wanapofika nyumbani kutoka shuleni." 

Kutokana na faida anayoipata katika ushonaji, Jeannette ameanzisha biashara ya pembeni, biashara ya mawese.  

Jeannette anaonekana akimfundisha msichana kushona na pia ana uhakika hata mvua zikiharibu tena cherehani yake, pesa anayoihifadhi kutokana na biashara ya mawese, anaweza kuikarabati. Na anashukuru akisema, "kama nisingekuwa na mkopo wa kutengeneza cherehani yangu, nisingefika popote na hali hii. Mvua ikinyesha tena, mafuriko huenda yakafuata tukasombwa." 

Audio Credit
Leah Mushi/Lucy Igogo
Photo Credit
FAO/Giulio Napolitano