Mlinda amani TANZBATT 7 nchini DRC anaeleza ratiba yake ya saa 24
Kila mara tumekuwa tukimulika shughuli za jumla za walinda amani wa Umoja wa Mataifa wanaohudumu katika maeneo mbali mbali duniani iwe ni ujenzi wa barabara, ulinzi wa amani na hata kilimo lakini leo tunaangazia je mlinda amani mmoja mmoja siku yake inakuwa vipi? Na leo tunammulika Luteni Kanali John Ndunguru, Kamanda wa kikundi cha 7 cha Tanzania, TANZBATT 7, kwenye kikosi cha kujibu mashambulizi, FIB cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, MONUSCO. Anayetuletea ripoti hiyo ni Issa Mwakalambo, Afisa Habari wa TANZBATT 7.
Uongozi imara na madhubuti wa Kamanda kikosi Luteni Kanali John Ndunguru wa kikundi cha 7 cha walinda amani kutoka Tanzania,TANZBATT 7) kinachohudumu katika Ujumbe wa Umoja wa Mataifa katika kikosi cha kujibu mashambulizi (FIB) MONUSCO nchini DRC, jimboni kivu kaskazini, umeleta mafanikio makubwa katika uwajibikaji wa maafisa na askari wa kikosi hicho.
Luteni Kanali Ndunguru anaeleza namna anavyofanya kazi zake ili kuhakikisha maafisa na askari wa kikundi hicho wanatekeleza majukumu yao kwa kufuata mila na desturi za Jeshi la Wananchi wa Tanzania na taratibu zilizowekwa na Umoja wa Mataifa katika maeneo wanayohudumu.
Pamoja na majukumu mengine ya msingi ambayo Kamanda Kikosi huyafanya, suala la michezo limepewa kipaumbele ili kuwawezesha walinda amani hao kuwa timamu kimwili na kiakili.
Tanzania imekuwa ikishiriki katika ulinzi wa amani hapa DRC kwa takriban vipindi saba hadi hivi sasa.