COVID-19 imesababisha ongezeko la vifaa tiba bandia duniani-UNODC
Ongezeko la ghafla la mahitaji ya dawa na vifaa tiba vya kukabiliana na janga la virusi vya corona au COVID-19 limesababisha ongezeko la usafirishaji haramu wa dawa na vifaa visivyo na viwango vinavyostahili au bandia kwa mujibu wa ripoti ya utafiti iliyochapishwa na ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na madawa na uhalifu UNODC. Taarifa inasomwa na Jason Nyakundi.
Ripoti hiyo iliyotolewa na UNODC hii leo mjiini Vienna Austria inasema “janga la COVID-19 limedhihirisha mapungufu yaliyopo katika mfumo wa sheria na ufuatiliaji wenye lengo la kuzuia utengenezaji na usafirishaji haramu wa bidhaa hizo ambazo ni tishio kubwa kwa afya ya umma.”
Akizungumzia changamoto hiyo mkurugenzi mtendaji wa UNODC Ghada Waly amesema “Afya na maisha ya watu yako hatarini wakati wahalifu wakitumia fursa ya janga la COVID-19 kujineemesha kwa fedha kutokana na hamasa ya watu na mahitaji ya vifaa vya kujikinga au PPE. Makundi ya kimataifa ya uhalifu wa kupangwa yanatumia mwanya uliopo katika mifumo ya ufuatiliaji ya kitaifa kuingiza dawa na vifaa badindia visivyokidhi viwango.”
Ameongeza kuwa “tunahitaji kuzisaidia nchi kuongeza ushirikiano ili kuziba mapengo, kuvijengea uwezo vyombo vya usalama na mfumo wa haki na sheria na kuelimisha umma kuhakikisha watu wako salama.”
Ripoti hiyo imesema magenge ya uhalifu wa kupangwa yameitumia hali ya sintofahamu inayozingira janga la COVID-19 kwa kuziba pengo la mahitaji ya madawa na vifaa tiba ambavyo ni haba na hivyo kusambaza vilivyo na viwango dunia au bandia.
Vifaa tiba bandia vina athari kubwa na mbaya kwa afya ya umma kwa kuwa huenda visitibu ipasavyo maradhi na vinaweza kuchangia hali ya dawa kuwa sugu mwilini imeongeza ripoti.
Ushahidi uliopo
Ushahidi wa ripoti unaonyesha kuwa matukio haramu kama vile udanganyifu, utapeli na kukusanya vitu vinavyohusiana na uzalishaji na usafirishaji haramu wa bidhaa zisizo na viwango vinavyostahili au bandia umeongezeka kufuatia kusambaa kwa virusi vya corona.
Ikitoa mfano ripoti imesema mathalani katika kisa kimoja hivi karibuni mamlaka ya afya ya Ujerumani ilitoa tenda kwa kampuni mbili nchini Uswisi na Ujerumani kupitia kwenye mtandao wa makampuni hayo ili kutengeneza barakoa zenye thamani ya euro milioni 15 na baadaye ikabainika kwamba kumbe mtandao si wao lakini ni wa kampuni halali na inayojulikana ya nchini Hispania na kampuni hizo zimeutumia kiharamu kujipatia kipato.
Ukurasa kuhusu virusivyacorona & taarifa mpya
Wasomaji wanaweza kupata taarifa na muongozo kuhusu mlipuko wa virusi vya corona (2019-nCoV) kutoka Umoja wa Mataifa, Shirika la afya duniani na mashirika mengine ya UN hapa. Kwa habari mpya kila siku kutoka UN News, bofya hapa.Pia ripoti imesema wakati huu wa COVID-19 kumeshuhudiwa takwimu za uongo na uhalifu ikiwemo kutumia barua pepe bandia, kurubuni watu na biashara bandia wahalifu wakitumia wavuti za makampuni yanayofahamika na kushawishi wanunuzi kuwa wato ni makampuni halali.
Mabadiliko katika uhalifu wa kupangwa
Ripoti hiyo ya UNODC pia inatabiri kwamba tabia ya magenge ya uhalifu wa kupangwa itabadilika taratibu katika kipindi cha janga hili hususan wakati ambapo chanjo itapatikana na magenge hayo huenda yakabadili mwelekeo kutoka kusafirisha kiharamu PPE na kuingia katika kusafirisha chanjo.
Mashambulizi ya mtandaoni dhidi ya miundombinu muhimu ya kushughulikia janga hili huenda yakaendelea katika mfumo wa utapeli mtandaoni ukilenga mamlaka za afya.
Hivyo ripoti inapendekeza kuwa kuimarisha mifumo ya sheria na faini na kuwa na mtazamo wa kimataifa wa kuharamisha utengenezaji na usafirishaji haramu wa vifaa tiba dunia au bandia ni muhimu kwani ni mtazamo wa Pamoja pekee ndio utawezesha kukabiliana na uhalifu huo unaoathiri watu na afya ya umma.
Lakini pia watu wanaofanya kwenye sekta ya afya watahitaji ujuzi mpya wa ziada kuweza kukabiliana na utapeli na uhalifu huo.