Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Burkina Faso ombi la UNHCR kwa wakimbizi lajibiwa

Burkina Faso ombi la UNHCR kwa wakimbizi lajibiwa

Pakua

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR, limefikisha tani 88 za misaada ya dharura kwa ajili ya wakimbizi kutoka nje na wakimbizi wa ndani nchini Burkina Faso. 

Ndege aina ya Boeing 777 iliyobeba shehena hiyo kutoka kituo cha kimataifa cha hifadhi ya misaada ya kibinadamu mjini Dubai, falme za kiarabu iliwasili mji mkuu wa Burkina Faso, Ouagadougou ambapo ndege hiyo ilikodishwa na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa Falme za Kiarabu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum.


Shehena hii ya karibuni zaidi inajumuisha makaratasi ya nailoni 21,300 yatakayotumika kwa makazi pamoja na kuimarisha nyumba 30,000 za  waliolazimika kukimbia na ni  msaada wa kwanza kufuatia ombi la UNHCR la dola milioni 186 kwa wakimbizi wa ukanda wa Sahel lililozinduliwa wiki mbili zilizopita kwa lengo  la kusaidia wakimibizi.


UNHCR inasema kuwa ghasia nchini Burkina Faso imesababisha watu zaidi ya 900,000 kukimbia makazi yao nchini humo ilhali taifa hilo la Afrika Magharibi tayari linahifadhi wakimbizi 21,000 waliokimbia machafuko nchini Mali.


Hivi sasa mazingira ya wakimbzi hao ni magumu, wengi wakilazimika kulala kwenye maeneo yasiyo rafiki ikiwemo malazi ya kuhamahama.


Shirika hilo linasema pia kuanza kwa msimu wa mvua, ambao mwaka huu unaambatana na pepo na mvua kali, vinazidi kuongeza mahitaji ya makazi.


Takribani wakimbizi 70,000 hivi sasa wanaishi kwenye maeneo yaliyo hatarini kufurika maeneo ya kaskazini kati na Sahel nchini Burkina Faso.


UNHCR na wadau wake hivi sasa wanakadiria kuwa wakimbizi hao wa ndani na wa kutoka nje wanahitaji msaada ambapo hadi sasa shirika hilo limetengeneza makazi 10,000.
 
 

Audio Credit
Loise Wairimu
Audio Duration
1'52"
Photo Credit
WFP/Mahamady Ouedraogo