Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF yachukua hatua kukabiliana na ukatili wa kingono Sierra Leone

UNICEF yachukua hatua kukabiliana na ukatili wa kingono Sierra Leone

Pakua

Nchini Sierra Leone taifa lililopitia vita vya wenyewe kwa wenyewe na kushuhudia vitendo vingi vya kikatili ukiwemo ukatili wa kingono, hata baada ya vita hivyo inaonekana jinamizi la ukatili bado linawasakama kama alivyobaini balozi mwema wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF. Tupate maelezo zaidi na John Kibego.

Katika mji wa Makeni nchini Sierra Leone balozi mwema wa UNICEF Ishmael Beah amepata fursa ya kutembelea eneo hili na kuzunguza na baadhi ya watoto waathirika wa ukatili wa kingono ambao bado unaendelea nchini humo na kusikiliza hadithi zao . Miongoni mwao ni binti huyu ambaye alipitia ukatili huo ambao asilani hatousahau mikononi mwa mwana jamii akiwa na umri wa miaka saba tu, anasimulia ilivyokuwa

Nilikuwa nimetoka mahali na mtu huyo akaniita na kuniambia niende kumnunulia sigara, kisha baadaye akanitaka kuingia chumbani kwake lakini nilikataa. Ndipo akanilazimisha kwa nguvu kuingia chumbani kwake, akanivua chupi na akaanza kuingiza vidole vyake katika sehemu zangu za siri, nilisikia mauamivu sana, niliumia. Baadaye nikaenda nyumbani na kumsimulia dada yangu kilichonisibu naye alisubiri mama arejee nyumbani na kuripoti tukio hilo. Mama yangu alinipeleka moja kwa moja hospitali na baada ya hapo tunaenda polisi na kuripoti tukio hilo."

Kwa balozi mwema Ishmael hili limemtia uchungu sana sio tu kwa kuwa ni baba wa watoto wawili wa kike lakini pia kwa kuona kwamba watu ambao wanastahili kuwalinda watoto ndio wanawageuka na kuwafanyia ukatili huo wakiwemo walimu na walezi katika jamii

”Kama baba imenikasirisha sana na kunitia huzuni, lakini pia imenitia hasira kwama mambo haya yapo. Najua sasa kumekuwepo na dharura ya kitaifa kuhusu hali hii na kumewekwa sheria za kuwawajibisha watu na kuwafunga, kwa mfano mwalimu sasa yuko jela, hivyo ni vizuri lakini nadhani juhudi zaidi zinahitajika kuhakikisha kuna sheria kali ili asiwepo mzazi yeyote ambaye atasita kumpeleka mwanaye shule”.

Hivi sasa UNICEF inashirikiana na wadau na serikali kuchukua hatua madhubuti sio tu za kuweka bayana ukatili huu ambao unafanyika nchi zima lakini pia kuitaka serikali ya sierra Leone kuweka sheria kali za uwajibishwaji na kuhakikisha hakuna mtoto mwingine yeyote atakayeupitia ukatili huu.

Audio Duration
2'29"
Photo Credit
UNICEF/UN0118457/