Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatma ya watoto milioni 370 iko njia panda kisa? COVID 19:UNICEF/WFP

Hatma ya watoto milioni 370 iko njia panda kisa? COVID 19:UNICEF/WFP

Pakua

Mustakbali wa watoto milioni 370 uko njiapanda kwa sababu ya janga la virusi vya corona au COVID-19 lililosababisha kufungwa kwa shule zilizokuwa mkombozi wa lishe yao imesema taarifa ya mashirika ya Umoja wa Mataifa iliyotolewa leo.

Katika shule ya mfalme George wa nne wanafunzi wakionekana kuwa na furaha sio tu kwa sababu ya masomo bali pia kutokana na mlo waliokuwa wakipatiwa bure shuleni kila siku , mlo ambao sasa ni vigumu kuupata kwani shule zimefungwa kutokana na COVID-19,

Mashirika ya Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF na la mpango wa chakula duniani WFP yanasema mlo huo kwa watoto wengi ulikuwa ndio mlo pekee wa siku hivyo  janga la COVIDI-19 limeongeza tatizo la njaa kimataifa na hususan miongoni mwa watu masikini.

Sasa yanazitaka serikali kuchukua hatua kuzuia janga la afya na lishe kwa watoto hao milioni 370 wanaokosa mlo sababu ya shule kufungwa.

Akisistiza hilo mkurugenzi mtendaji wa WFP David Beasley amesema “Kwa mamilioni ya watoto kote duniani mlo wanaoupata shuleni ndio mlo pekee wa siku hiyo na bila mlo huo basi wanashinda njaa, wanakuwa kwenye hatari ya kuugua, wanaacha shule na kupoteza fursa nzuri ya kuukwepa umasikini. Ni lazima tuchukue hatua sasa kuzuia zahma ya kiafya kuwa janga kubwa la njaa.”

Kwa wasichana mashirika hayo yanasema mlo shuleni ni muhimu sana kwani katika nchi nyingi masikini ahadi ya kupata mlo shuleni inatosha kuwafanya wazazi wasiojiweza kupeleka binti zao shuleni na hivyo kuwaepusha na kazi ngumu za majumbani au ndoa za mapema.

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa UNICEF Henrietta Fore amesema Shule ni zaidi ya mahali pa kusoma , kwa watoto wengi ni mahali pa kuwahakikishia usalama, huduma za afya na lishe.Tusipochukua hatua sasa kuongeza huduma za kuokoa maisha basi athari za COVID-19 zitashuhudia katika miongo kadhaa ijayo.”

WFP na UNICEF katika miezi ijayo zitazisaidia serikali kuhakikisha kwamba wakati shule zinafunguliwa watoto watafaidika na program za mlo shuleni, afya na lishe na pia kufuatilia kwa pamoja watoto wanaohitaji mlo shuleni kupitia ramani maalum mtandaoni iitwayo School Meals map.

Mashirika hayo yametoa ombi la dola milioni 600 ili kujikita kwanza na nchi 30 masikini kuwasaidia watoto milioni 10.

Audio Duration
2'18"
Photo Credit
WFP/Challiss McDonough