Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanawake tusirudi nyuma katika ulinzi wa amani- Rubani Valentina

Wanawake tusirudi nyuma katika ulinzi wa amani- Rubani Valentina

Pakua

Takwimu zinaonesha kuwa zaidi ya walinda amani 200 wa Umoja wa Mataifa wamepoteza maisha katika moja ya nchi hatari duniani ya Mali. Marubani wanawake ni miongoni mwa walinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini humo wanaopiga doria zaidi katika eneo la kaskazini mwa Mali ambalo ni jangwa kufuatilia vikosi katili na pia kusaidia kutunza makubaliaono ya amani ambayo yako katika hali tete. Tupate maelezo Zaidi na Arnold Kayanda

Hii ni video inayorekodiwa kutoka angani katika helikopta, katika eneo la jangwa huko Kaskazini mwa Mali.

Jangwa kubwa la nchi ya Mali liko katika tishio kutoka kwa makundi ya wanamgambo. Walinda amani 13,000 wanalinda mkataba wa amani kati ya serikali na muungano wa vikundi viwili vyenye silaha.

Helikopta zinatoa msaada muhimu wa uchunguzi na pia operesheni za ardhini kote nchini.

Kapteni Valentina Iglesias aliungana na mpango wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Mali MINUSMA mnamo mwaka 2018. Yeye ni mmoja wa walinda amani 90 kutoka El Salvador wanaohudumu katika MINUSMA.

(Sauti ya Kapteni Valentina)

“Hii ni fursa ambayo si mara zote unaweza kuwa nayo. Kwa hivyo ninajaribu kufanya kila ninaloweza kwenye huu uzoefu na pia kuiwakilisha nchi yangu vizuri. Na kujiwakilisha mwenyewe kama mwanamke.”

Kapteni Iglesias ni rubani wa pili wa kike wa Helikopta, anayehudumu MINUSMA nchini Mali. Mpango unaosema wanawake wametoa mchango muhimu katika mafanikio ya mpango wa ulinzi wa amani

(Sauti ya Kapteni Valentina)

“Ninajihisi kuchangamana katika kundi. Wafanyakazi wenzangu hawanioni kuwa wa tofauti kwa kuwa mimi ni mwanamke katika mpango huu. Na hiyo haiathiri kazi yangu. Kwa hivyo najisikia vizuri kwasababu ninajihisi mimi ni miongoni mwa timu na sitakiwi kuwa na mipaka katika kazi ninazozifanya eti kwa kuwa mimi ni mwanamke. Ninaanza kuzoea kuwa mbali kwasababu sijawahi kuwa mbali na familia yangu bila kuwaona. Hivyo ninajaribu kujifunza kukabiliana na umbali. Ni ngumu kiasi lakini ninawasiliana nao kupitia ujumbe mfupi au video. Si mara zote tunafahamu kuhusu mambo yalivyo ardhini kwa hivyo wakati wote kuna hatari katika kila kazi tunayofanya. Ndiyo ni hatari kiasi lakini haizuii kuwa ya kufurahisha.”

Kapteni Valentina anatoa wito kwa wanawake wote kutosita wanapoitwa kushiriki katika shughuli za ulinzi wa amani.

Audio Duration
2'23"
Photo Credit
MINUSMA/Harandane Dicko