Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mradi wa UNHCR wa usaidizi wa makazi waleta nuru kwa wakimbizi wa Sudan Kusini nchini Kenya

Mradi wa UNHCR wa usaidizi wa makazi waleta nuru kwa wakimbizi wa Sudan Kusini nchini Kenya

Pakua

Msaada wa fedha katika makazi ya wakimbizi ya Kalobeyei nchini Kenya unawaruhusu wakimbizi kujenga nyumba zao kwa kutumia vifaa vya ujenzi wanavyovinunua kutoka kwa jamii za wenyeji kupitia programu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR inayowasaidia wakimbizi na wenyeji wao.

Florence amefurahi. Ana makazi mapya. Hapo awali alikuwa anaishi katika hema na watu wengine kumi na wawili akisema kuwa, “lilikuwa na msongamano sana na pia joto sana. Tuliishi kwenye hema kwa miaka miwili. Sasa tuna makazi ya kudumu na sasa hali imebadilika na kuwa nzuri. Ninajihisi furaha. Unaiangalia  nyumba yako iko tofauti. Unajisikia vizuri ukiwa ndani.” 

Wakimbizi wanapokea msaada wa fedha kupitia kadi maalumu za ATM. Moffat Kamau ni afisa mwandamizi wa UNHCR katika mpango huo wa fedha anasema,“mchakato huu unawaleta pamoja wakimbizi na jamii wenyeji kwasababu wakimbizi wanakuwa na uwezo wa kununua vifaa kutoka kwa msambazaji yeyote. Wasambazaji wengi kwa sasa ni jamii wenyeji na wajenzi ni wakimbizi na pia jamii wenyeji.”

Florence anategemea kupata mtoto wake wa tano na ana mipango mikubwa kwa siku zijazo na kwamba, “nataka mstakabali wa watoto uende mbele. Nitatumia vizuri fedha hii kujenga nyumba nyingine.Ninafurahi. ”

Audio Credit
Assumpta Massoi/Arnold Kayanda
Audio Duration
1'29"
Photo Credit
Picha/UN-Habitat/Julius Mwelu