Nigeria na Ethiopia zachomoza kwenye kuvutia mitaji ya kigeni- UNCTAD
Mwaka 2030 ambao ni ukomo wa malengo ya maendeleo endelevu, SDGs, hauko mbali. Umoja wa Mataifa kila uchao unaendelea na tathmini kuona lipi linapaswa kufanyika ili ahadi hiyo yenye malengo 17 iweze kufanikiwa na mafanikio hayo yawe na manufaa kwa kila mkazi wa sayari ya dunia. Harakati hizo zimesongeshwa wiki hii kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani ambapo Rais wa Baraza kuu aliitisha kikao kuangazia je mitaji kwenye uwekezaji inakwenda au ndio kusuasua? Kamati ya Umoja wa Mataifa ya biashara na maendele, UNCTAD, ndio msimamizi wa masuala ya uwekezaji na Katibu wake Mkuu Dkt. Mukhisa Kituyi alikuwa mmoja wa watoa mada kuu. Assumpta Massoi alimuuliza kulikoni mkutano huo wakati huu, na hapa kwenye makala hii anaanza kwa kujibu swali hilo.