Madai ya ukatili wa kingono dhidi ya mlinda amani, uchunguzi waanza
Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini-UNMISS umeanza uchunguzi kuhusu madai dhidi ya mlinda amani mmoja ya kumnyanyasa kingono msichana mmoja wa kisudan mjini Aweil nchini Sudan Kusini.
Taarifa ya UNMISS inadai kuwa mlinda amani huyo kutoka Nepal alimnyanyasa kingono mmoja kati ya wasichana wane waliokamatwa wakijaribu kuingia kwenye kambi ya Umoja wa Mataifa mjini Aweil kinyume cha sharia.
Yadaiwa kuwa baada ya kumfanyika kitendo hicho mlinda amani huyo alimpatia fedha huku ikielezwa bayana kuwa hakukuwepo na kitendo chochote cha ubakaji.
Tayari ofisi inayohusika na masuala ya unyanyasaji wa kingono-IRT huko Aweil inakusanya taarifa muafaka pamoja na kuhifadhi ushahidi ili kuweza kushughulikia uchunguzi kamili wa tukio hilo , ambapo uchunguzi utafanywa na Nepal ambako ndiko anatoka mlinda amani huyo.
Nayo ofisi ya huduma ya masuala ya uchunguzi wa ndani ya Umoja wa Mataifa-OIOS imearifiwa sambamba na Nepal ambako anatoka askari huyo.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres vitendo vya ukatili wa kingono katu havitavumiliwa na chombo hicho na UNMISS imesema imeazimia kutanguliza haki za msichana husika kwa kuweka wazi na kuwajibika kuhusu tukio hilo.