Vikosi vya usalama DRC vinatumia nguvu kupindukia -UN
Ripoti hiyo iliyotolewa leo katika miji ya Geneva na Kinshasa, inaorodhesha mauaji na ukiukwaji mwingine wa haki za binadamu uliofanywa na vikosi vya usalama katika mazingira ya kuzima maandamano.
Ripoti inasema kuna ishara kwamba vikosi vya usalama vya DRC vimejaribu kufunika ukiukwaji huo kwa kuondoa miili ya waathirika na pia kuzuia kazi za wachunguzi wa kitaifa na kimataifa.
Mjumbe maalum wa katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, Leila Zerrougui amesema ripoti inamulika mapengo ya kutowajibika, muendelezo wa kudidimiza demokrasia katika nchi ambayo imekuwa ikichunguzwa tangu mwanzo wa mwaka 2015, akisema
“Hii inakwenda kinyume na makubaliano ya mkataba wa Disemba 31 mwaka 2016 na hatua zake za kujenga imani. Maandamano yanambatana na uhuru wa kujieleza na ni muhimu kuwa sauti zote zisikilizwe katika muktadha wa uchaguzi mkuu ujao.,”
Ripoti ambayo imechapishwa kwa pamoja na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za Binadamu pamoja na ile ya kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa mataifa nchini DRC-MONUSCO inaeleza kutoheshimu misingi ya sheria za kitaifa na kimataifa, hasahasa ile misingi ya uhalali, mahitaji, kiasi gani cha kutumia, tahadhari na uwajibikaji ambavyo vinahusika na matumizi ya nguvu na vikosi vya usalama wakati wa kukabiliana na maandamano ya amani kati ya januari 2017 na januari ya mwaka 2018.