Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali ya kibinadamu Syria bado ni mateso matupu- Mueller

Hali ya kibinadamu Syria bado ni mateso matupu- Mueller

Pakua

Msaidizi wa Katibu  Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya kibinadamu na msaada wa dharura, Ursula Mueller, amesema hali bado ni tete nchini Syria kufuatia mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yaliyodumu kwa zaidi ya miaka saba sasa.

Katika taarifa yake kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hii leo kuhusu Syria, Bi. Mueller amesema mgogoro huo umesababisha mateso makubwa  kwa wananchi, vifo vingi kwa raia na huku wengine wakijeruhiwa au kutojulikana waliko.

Umoja wa Mataifa  unakadiria kuwa watu  milioni 13.1 wanahitaji ulinzi pamoja na msaada  wa kibinadamu.

Miongoni mwao milioni 6.1 hawana makazi nchini mwao na wengine  milioni 5.5 wametorokea nchi jirani.

Bi. Mueller ameliambia Baraza la Usalama kuwa wakati huu mapigano yakiwa yanaendelea ana wasiwasi na maisha ya raia wa kawaida ambao wamejikuta katikati ya mapigano kaskazini Mashariki mwa Syria ambako uhasama unaoendelea unaripotiwa kusababisha  vifo pamoja na majeruhi kadhaa.

image
Mtoto mkimbizi kutoka Syria akikabiliana na baridi kali na theluji kwenye kambi yao huko Lebanon. (Picha:© UNICEF/Romenzi)
Pia amesema kuwa mji wa Raqqa baado si salama kwa raia na  ana wasiwasi kuwa watu sasa wanaendelea kurejea katika mji huo licha ya kuwa kuna mabomu yaliyotapakaa ambayo hayakulipuka.

Takriban watu 60,000 wamerejea mjini humo tangu kumalizika kwa mapigano Oktoba mwaka 2017.

Wakati huo huo, akizungumza kwa njia ya video kutoka mjini Sochi, Urusi ambako mkutano kuhusu Syria unaendelea, Mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Syria Staffan de Mistura amesema

(Sauti ya Staffan de Mistura)

"Tumekubaliana kuunda kamati ya katiba itakayojumuisha serikali, upinzani na washiriki huru ili kuandaa rasimu ya katiba kwa misingi ya azimio la Baraza la Usalama namba 2254. Tuliweza kujumuisha kwenye azimio la mwisho la mkutano wa majadiliano wajibu wa wote kwamba lengo la yote tunayojaribu kufanya ni kutekeleza kikamilifu azimio la Baraza la Usalama.”

image
Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Syria Staffan de Mistura akihutubia kwa njia ya video (Picha:UN/Kim Haughton)
Photo Credit
Mtoto mkimbizi nchini Syria akipatiwa huduma ya matibabu. (Picha: © UNICEF/NYHQ2014-1193/Rashidi)