WHO na UNEP kushirikiana kuboresha afya
Pakua
Mashirika ya mawili ya Umoja wa Mataifa yamekubaliana kushirikiana kuchagiza hatua dhidi ya athari za afya ya kimazingira zinazosababisha vifo vya zaidi ya watu milioni 12 kila mwaka.
Mashirika hayo ni lile linaloshughulikia mazingira la UN- Environment na la afya, WHO.
Mkataba wa ushirikiano umetiwa saini leo mjini Nairobi kati ya vinara wa mashirika hayo, Erik Solheim wa UN Environment na Dkt Tedros Adhanom Ghebreyesus wa WHO.
Makubaliano yamejikita katika kuongeza hatua za kupambana dhidi ya uchafuzi wa hali ya hewa, tabianchi pamoja na kuboresha uratibu wa kusimamia vema kemikali pamoja na taka.
Pia masuala ya ubora wa maji safi, chakula na lishe nayo hayakupigwa kisogo.
Ingawa mashirika haya mawili yamekuwa yakishirikiana katika nyanja mbalimbali, lakini ushirika huu mpya una umuhimu wake kwani hii ndiyo mara ya kwanza, kwa kipindi cha miaka 15, kuweza kushirikiana katika masuala ya afya pamoja na mazingira.
Akizungumza katika hafla hiyo, mkuu wa shirika la mazingira, Bwana Solheim, amesema kuwa , kuna haja ya mashirika hayo mawili kuharakisha ushirikiano wao ili kuweza kushughulikia tisho la mazingira pamoja na hali ya hewa.
Yeye mwenzake wa shirika la WHO, Dkt Tedros, amesema kuwa afya yetu ina mafungamano ya karibu na mazingira ya binadamu.
Ameongeza kuwa kwa pamoja hatari ya hewa, maji pamoja na kemikali husababisha vifo vya watu zaidi ya millioni 12 kila mwaka hutokea katika mataifa yanayonukia katika mabara ya Asia, Afrika na Amerika Kusini ambako vifo vingi huchochewa na uchafuzi wa mazingira.
Aidha amesema kuwa hili halikubaliki haliwezi kuendelea.