Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO na UNEP kushirikiana kuboresha afya

WHO na UNEP kushirikiana kuboresha afya

Pakua

Mashirika ya mawili ya Umoja wa Mataifa  yamekubaliana kushirikiana  kuchagiza hatua dhidi ya athari za afya ya kimazingira  zinazosababisha vifo vya zaidi ya watu milioni 12 kila mwaka.

 
Mashirika hayo ni lile linaloshughulikia mazingira la UN- Environment na la afya, WHO.
 
Mkataba wa ushirikiano umetiwa saini  leo mjini Nairobi kati ya vinara  wa mashirika hayo, Erik Solheim wa UN Environment na  Dkt Tedros Adhanom  Ghebreyesus wa WHO.
 
Makubaliano yamejikita katika kuongeza  hatua za kupambana dhidi ya  uchafuzi wa  hali ya hewa, tabianchi pamoja na kuboresha uratibu wa  kusimamia vema kemikali pamoja na taka.
 
Pia masuala ya ubora wa maji safi, chakula na lishe nayo hayakupigwa kisogo.
 
 Ingawa mashirika haya mawili yamekuwa yakishirikiana katika nyanja mbalimbali, lakini ushirika huu mpya una umuhimu wake kwani hii ndiyo mara ya kwanza, kwa kipindi cha miaka 15, kuweza  kushirikiana  katika masuala ya afya pamoja na mazingira.
 
Akizungumza katika hafla hiyo, mkuu wa shirika la mazingira, Bwana Solheim, amesema kuwa , kuna haja ya mashirika hayo  mawili kuharakisha ushirikiano wao  ili kuweza kushughulikia  tisho la mazingira pamoja  na hali ya hewa.
 
Yeye mwenzake wa shirika la WHO, Dkt Tedros, amesema kuwa afya yetu ina mafungamano ya karibu na mazingira ya binadamu.
 
Ameongeza kuwa  kwa pamoja  hatari ya  hewa, maji pamoja na kemikali husababisha vifo vya watu zaidi ya millioni 12 kila mwaka  hutokea katika  mataifa yanayonukia katika mabara ya Asia, Afrika na Amerika Kusini ambako vifo vingi huchochewa  na uchafuzi wa mazingira.
 
Aidha amesema kuwa  hili halikubaliki haliwezi kuendelea.
Photo Credit
UNEP na WHO kushirikiana kuboresha afya. Picha: UM/Video capture