Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Shule ya msingi Zimbabwe yashinda tuzo ya elimu kwa kilimo endelevu

Shule ya msingi Zimbabwe yashinda tuzo ya elimu kwa kilimo endelevu

Pakua

Nchini Zimbabwe shule moja ya msingi imeshinda tuzo ya elimu kwa maendeleo endelevu kutokana na mfumo wake wa kilimo kinachohifadhi mazingira na wakati huo huo kujipatia kipato.

Shule hiyo iitwayo Sihlengeni iliyoko wilaya ya Umzingwane, kwenye jimbo kame zaidi la Matebele imeshinda tuzo hiyo iambatanayo na donge nono la dola 50,000 inayotolewa kwa pamoja na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni, UNESCO na serikali  ya Japan.

Kupitia mradi wa upandaji miti ya matunda, bustani ya mazao yenye lishe,uimarishaji misitu na ufugaji, shule hiyo imegeuka kuwa kijito ambapo wanafunzi na walimu wanapata stadi ambazo huzitumia hata makwao na kujipatia kipato.

Mwalimu Mkuu Sibanga Ncube ambaye pia ni meneja wa mradi huo amesema umehusisha walimu 17 na wanafunzi 738 ambao nao huko makwao wameshirikisha wazazi wao.

Mradi ulianza mwaka 1995 baada ya shule kupatiwa mafunzo ya kilimo endelevu ambao unazingatia kuhifadhi mazingira asili ya eneo husika sambamba na kulinda mazingira.

Bwana Ncube amesema hivi sasa wageni wanastaajabu kuona eneo lililokuwa kame sasa limesheheni matunda kama vile machunga, mapapai, na nyanya kilimo ambacho nao pia wanataka kutekeleza huko makwao.

Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO pamoja na Waziri wa Elimu wa Japan watakabidhi washindi hao tuzo hiyo katika hafla itakayofanyika makao makuu ya shirika hilo huko Paris, Ufaransa tarehe 3 mwezi ujao.

Photo Credit
Green Oasis_shule ya msingi ya Sihlengeni_Zimbabwe. Picha: © Sihlengeni Primary School