Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dola milioni 253 zasakwa kuimarisha haki duniani

Dola milioni 253 zasakwa kuimarisha haki duniani

Pakua

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imezindua ombi la dola milioni 253 ili kusaidia kuimarisha haki za binadamu maeneo mbali mbali duniani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Kamishna Mkuu wa haki za binadamu Zeid Ra’ad Al Hussein amesihi wahisani wachangie ili kuimarisha kazi za ofisi yake ya kusimamia haki,hasa wakati huu ambapo mustakhbali wa haki duniani uko mashakani.

Amesema katika nchi nyingi hata sheria sasa zinashambuliwa, wageni wakikumbwa na chuki huku ubaguzi kwa misingi ya kidini na rangi ukiwa ni hoja za kila uchao.

Kamishna Zeid amesema kushindwa kwa pamoja kupunguza au kusaka suluhu ya mizozo kunazidi kuchochea vikundi vyenye misimamo mikali vinavyozidisha machungu kwa mamilioni ya watu, wengi wakilazimika kukimbia makwao.

Amekumbusha kuwa uwekezaji katika haki za binadamu hii leo, kutakuwa ni kinga dhidi ya ukiukwaji wa haki hapo kesho.

Photo Credit
Kamishina Mkuu wahaki za binadamu Zeid R'aad Al-Husein. Picha na UM/Jean MarcFerre