Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Shambulio nchini Mali, watu 60 wauawa wengine wamejeruhiwa

Shambulio nchini Mali, watu 60 wauawa wengine wamejeruhiwa

Pakua

Watu 60 wameuawa na wengine makumi kadhaa wamejeruhiwa katika shambulio lililotokea asubuhi huko Gao nchini Mali kwenye kambi ya watendaji wa kusimamia mchakato wa amani nchini humo.

Mkuu wa operesheni za ulinzi wa amani kwenye Umoja wa Mataifa Herve Ladsous ametoa taarifa hizo leo jijini New York, Marekani wakati wa kikao cha Baraza la Usalama kilichokuwa kinajadili hali ya usalama nchini Mali.

(Sauti ya Ladsous)

“Lazima tuchunguze na kubaini kilichotokea, lakini tunachofahamu ni kwamba gari lililokuwa na vilipuzi lililipuliwa ndani ya kambi yenyewe.”

Akizungumzia kambi hiyo iliyoko Gao, Ladsous amesema..

“Takribani watu 600 kutoka kikundi cha uratibu wakiwemo wanajeshi wa Mali walikuwa wamekusanyika wakijiandaa kwa doria za pamoja.”

Bwana Ladsous amesema shambulio hilo la leo linazidi kupatia chepuo utekelezaji wa mkataba wa amani kama njia pekee ya kufanikisha mchakato wa amani na hatimaye kuleta utulivu nchini Mali

Amesema Umoja wa Mataifa kwa upande wake utaendelea kusimama kidete na wananchi wa Mali ili kusaidia serikali yao na pande zilizosaini mkataba huo kuutekeleza kwa haraka.

Photo Credit
Walinda amani wa MINUSMA wakipiga doria nchini Mali.(Picha:Sylvain Liechti/MINUSMA)