Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

ICTY yamfutia mashitaka Vojislav Šešelj :

ICTY yamfutia mashitaka Vojislav Šešelj :

Pakua

Mahakama ya kimataifa ya mauaji ya kimbari ya Yugoslavia ya zamani ICTY leo imemfutia mashitaka yote na kumwachia huru Vojislav Šešelj, Rais wa chama cha Serbia cha Serbian Radical Party na mjumbe wa zamani wa bunge la Jamhuri ya Serbia. Vojislav Šešelj alikuwa anakabiliwa na mashitaka tisa ambapo matatu miongoni mwao ni ya uhalifu dhidi ya ubinadamu yakijumuisha mateso, kufukuzwa na vitendo vya kinyama vya uhamisho kwa nguvu.

Na sita yaliyosalia ni ya uhalifu wa vita ikiwemo mauaji, mateso na ukatili, uangamizaji, uharibifu au uharibifu wa makusudi uliofanyika kwa taasisi za kujitolea kwa ajili ya dini au elimu, uporaji wa mali ya umma au binafsi.

Alishutumiwa kuhusika na uhalifu huo uliotejkelezwa na vikosi vya Serbia kuanzia Agost mwaka 91 hadi Septemba mwaka 1993. Ukitolewa uamuazi dhidi yake Jaji Lattanzi wa mahakama hiyo amesema , upande wa mashitaka umeshindwa kuthibitisha madhumuni ya kuwepo kwa jinai, suala ambalo ni takwa la kisheria. Kesi yake ilianza 7 Novemba 2007 na imesikiliza mashahidi 99 , 90 wakiwakilisha upande wa mashitaka.

Photo Credit
Vojislav Šešelj: Picha na ICTY