Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mahitaji ya kibinadamu Syria yaongezeka kwa 2016, dola milioni 8 zahitajika

Mahitaji ya kibinadamu Syria yaongezeka kwa 2016, dola milioni 8 zahitajika

Pakua

Wakati vita nchini Syria vikielekea mwaka wa sita bila dalili ya ukomo wake, mashirika ya Umoja wa Mataifa ya kibinadamu na maendeleo yametoa wito kwa nchi wanachama wa Umoja huo zichangie ombi la dola bilioni 7.73 zinazohitajika kufadhili utoaji misaada kwa watu milioni 22.5 nchini Syria, na katika ukanda mzima mwaka 2016.

Ombi hilo la changisho linajumuisha mambo mawili: kwanza, ni kuwasaidia wakimbizi milioni 4.7 wanaotarajiwa katika nchi jirani kufikia mwishoni mwa mwaka 2016 na watu milioni 4 na jamii za wenyeji wao, na pili, kuwasaidia watu milioni 13.5 waliolazimika kuhama makwao na walioathiriwa na mzozo ndani ya Syria yenyewe.

Kamishna mpya wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR, Filippo Grandi, amesema ingawa sasa wimbi la wakimbizi wanaomiminika Ulaya hatimaye limeufanya ulimwengu kuumulika mzozo wa Syria na madhila ya kibinadamu unayoyazua, mzigo mkubwa zaidi wa wakimbizi hao unabebwa na jamii za watu binafsi na serikali za ukanda wa Mashariki ya Kati.

Amesema ni lazima ukomeshwe mwelekeo wa wakimbizi wa Syria kutumbukia katika umaskini hata zaidi, waongezewe matumaini ya mustakhbali wao wenyewe na nchi yao, na kuwasaidia wale wanaowapa hifadhi.

Photo Credit
Filippo Grandi. Picha ya UN/Evan Schneider